Jumatano, 22 Aprili 2015

SERIKALI KUPUNGUZA UTITIRI WA KODI


 Ni naibu waziri wa fedha na uchumi Mh. Mwigulu Nchemba, akisikiliza jambo katika sherehe ya uzinduzi wa Vicoba Day, vikundi vya kiuchumi vilivyopo katika jimbo la Mufindi kaskazini.
 Mwigulu Nchemba akiwa na naibu waziri wa maliasili na utalii, Mahamood Mgimwa, ambaye ni mbunge wa jimbo la Mufindi kaskazini- Iringa. katika uzinduzi wa "Vicoba Day"
 Mwigulu Nchemba akivikwa vazi maalumu la kusimikwa kuwa kiongozi bora.
 Mwigulu Nchemba (katikati) akiwa na Mahamood Mgimwa (kushoto) na Isaack Kaganga mlezi wa vicoba jimbo la Mufindi Kaskazini.
 Mwigulu Nchemba akitete jambo na kanal Mkisi kamanda wa kikosi cha jeshi la kujenga Taifa JKT Mafinga, na kulia ni mbunge wa Mufindi Kusini Mendrad Kigola- siku ya uzinduzi wa "Vicoba Day"
 Kanal Mkisi - kamanda wa jeshi la kujenga Taifa JKT Mafinga akimsikiliza Mwigulu Nchemba naibu waziri wa fedha.

<<<HABARI>>>

SERIKALI imekili uwepo wa utitiri wa kodi kwa mfanyabiashara, na kuwa sasa kuna mpango wa kurekebisha mifumo yake ya ukusanyaji wa kodi na ushuru mbalimbali ili kupunguza mbinyo uliopo, ambao unaowafanya baadhi ya wafanyabiashara nchi, kushindwa kuendesha shughuli zao.

Hatua hiyo inakuja wakati wafanyabiashara kote nchini wakitumia mbinu mbalimbali, ikiwemo njia ya kusitisha utoaji wa huduma kwa wananchi - kwa kufunga maduka, kwa lengo la kuishinikiza serikali kubadili mfumo wake wa ukusanyaji wa kodi, ikiwa pamoja na kupinga ongezeko la kodi kwa asilimia 100.


Hayo yamezungumzwa na naibu waziri wa fedha Mwigulu Nchemba, katika mkutano baina yake na wanachama wa vikundi vya benki za wananchi waishio vijijini Vicoba, katika siku ya uzinduzi wa “Vicoba day”- vikundi vilivyopo jimbo la Mufindi Kaskazini- Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.

Mwigulu amesema utitiri wa kodi uliopo sasa unadumaza shughuli za mfanyabiashara, kutokana na mgawanyiko wa ukusanyaji wa kodi hizo, huku akidai kuwa wizara yake imeitaka Tamisemi, na wizara ya viwanda na biashara kuondoa usumbufu uliopo unaoilazimu kila idara kukusanya kodi.

Aidha Mwigulu amesema sasa serikali imefuta mfumo wa awali uliokuwa ukitoa mwanya kwa matajiri kusamehewa kodi, na masikini wakibebeshwa mzigo huo wa ulipaji wa kodi, jambo ambalo halikuwa linatenda haki kwa wananchi.

“Ule utaratibu wa misamaha ya kodi kwa matajiri tumeifuta,..maana unakuta mtu anachimba mafuta halipi kodi, lakini mama anayeuza Dagaa au vitumbua asubuhi na mapema anabanwa alipe kodi, huu utaratibu wa kumbana masikini alipe kodi ili kumuhudumia tajiri tumeuondoa, tunataka kila mmoja alipe kodi anayostahili,” Alisema Mwigulu.

Amesema mfumo huo wa ulipaji kodi licha ya kuwa ni mzigo kwa masikini pia ulikuwa unajenga tabaka la watu wenyenacho na wasionacho, na kuwa serikali kupitia mikakati yake imeanza kuondoa tabaka hilo kwa kujenga shule za sekondari kila Kata.

….Amesema awali kabla ya shule za kata hazijajengwa, baadhi ya mikoa ilikuwa na idadi ndogo ya shule za sekondari na hivyo kukosekana kwa mwamko wa elimu kwa wananchi wa maeneo hayo.

Ameongeza kuwa mpango huo wa shule za sekondari kila kata na ujenzi wa Zahanati, utasaidia kuondoa tabaka lililopo la wenyenacho na wasionacho kwa kuwa kila mwananchi atakuwa na upeo mpana wa kufikiri namna ya kuzifikia fulsa za kiuchumi.


Pia amesema wizara yake haitawavumilia watumishi wa aina yoyote ambao hawatakuwa waaminifu kwa fedha za umma, na akitolea mfano idara ya afya, Mwigulu amesema huko  baadhi ya watumishi wanatabia ya kuchepusha dawa, ambazo zimelipiwa fedha na serikali kwa lengo la kuwahudumia wagonjwa.

“Wizara inatoa fedha kwa ajili ya kununua dawa, lakini mgonjwa akienda Hospitali anaambiwa dawa hakuna kanunue, hizi zilizolipiwa na serikali amekunywa nani? Na wakati mwingine kule bungeni tunabanwa tutoe hela za dawa, lakini hospitali au Zahanati dawa hakuna, nani kanywa hizi dawa?, alihoji Mwigulu.


Hata hivyo Mwigulu amesema atapambana na Halmashauri zote ambazo hazitengi asilimia 10 ya fedha za mapato yake ya ndani – kwa ajili ya makundi ya wanawake na vijana, na ili kudhibiti hali hiyo wale watakaokaidi agizo hilo watachukuliwa hatua za kinidhamu ikiwa pamoja na kuwafukuza kazi watumishi wa aina hiyo

Kuhusiana na masuala ya kiuchumi- Mwigulu amewahimiza wanachama wa Vicoba kutunza kumbukumbu za mahesabu yao ili waweze kupata mikopo katika taasisi za kifedha, na kuwa serikali ipo katika hatua za mwisho kuvitambua kisheria vikundi hivyo vya vicoba.

MWISHO.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni