Alhamisi, 13 Februari 2014

PSPF YATOA MISAADA KWA WAATHIRIKA IZAZI


 
 Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Izazi wakiteremsha misaada iliyotolewa na  mfuko wa pensheni kwa watumishi wa Umma PSPF, - katika gari ambalo limefika katika kijiji hicho kwa ajili ya kuwasadia baada ya kukumbwa na janga hilo la mvua kuleta uharibifu mkubwa wa mali na bidhaa mbalimbali
 Baadhi ya viongozi wa PSPF na Halmashauri ya Wilaya ya Iringa wakitazama wananchi wakiteremsha misaada hiyo kwa waathirika.
 Baadhi ya viongozi wa PSPF na wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa wakiwa wamenyanyua moja ya Godoro wakati wakikabidhi msaada huo kwa waathirika wa mvua Izazi.


 Moja kati ya Mabati 200 zilizotolewa na mfuko huo wa PSPF.

 Mjumbe wa bodi ya PSPF Bw. Peter Ilomo (mwenye shati nyekundu) akiwa na uongozi wa halmashauri ya Wilaya ya Iringa baada tu yakukabidhi msaada huo wenye thamani ya shilingi Milioni kumi. -Wakwanza kushoto ni  Steven Mhapa mwenyekiti wa H/W ya Iringa.
 Baadhi ya wananchi wa kijiji cha Izazi (Kushoto) wakishuhudia msaada wa vitu mbalimbali kutoka katika mfuko wa PSPF kama ni moja ya usaidizi kwa wananchi waliokumbwa na uharibufu wa mvua zilizoambatana na upepo mkali.


HATIMAYE mfuko wa pensheni kwa watumishi wa Umma PSPF umetoa msaada wa vitu vyenye thamani ya shilingi Milioni 10 kwa wananchi wa Kata ya Izazi Wilayani Iringa, ambao waliezuliwa nyumba zao baada ya mvua kubwa zilizoambatana na upepo mkali kuleta uharibifu.

akikabidhi msaada huo kwa waathirika wa janga hilo, Peter Ilomo ambaye ni mjumbe wa bodi ya PSPF Taifa na katibu mkuu ofisi ya rais Ikulu, amesema lengo la kutoa msaada huo ni kupunguza ukali wa maisha kwa wananchi waliokumbwa na tukio hilo.

Aidha PSPF  kupitia mwakirishi huyo wa kitaifa imekabidhi Mabati 200, Magodoro 50, Blanketi 98, Sukari kilo 50 pamoja na Misumari ya Bati Kg 100, msaada wenye thamani ya shilingi Milioni 10.

"Tunafahamu kuwa mlipatwa na janga kubwa na tumeangalia baadhi ya nyumba, taabu ambayo mmeipata na mnaendelea kuipata itachukua muda kabala haijapatiwa ufumbuzi wa kudumu, hata hivyo kama ilivyo desturi yetu watanzania na kama Mfuko wa PSPF tumeona tuje kuwasaidia japo kidogo kutatua tatizo mlilonalo japo hatuwezi kumaliza kabisa tatizo hilo," Alisema Ilomo.

Ilomo ameutaka uongozi utakaohusika na ugawaji wa msaada wa vitu hivyo kuhakikisha unatenda haki, ili vitu hivyo viwafikie walengwa pasipo kufanya uchepushaji ambao utaleta lawama siku za usoni.

"Niwaombe viongozi kuwa utaratibu utakaotumika katika kuvigawa vitu hivi uwe ni utaratibu wa wazi  ili usilete manung'uniko katika msaada, kwani msaada unapotolewa inatakiwa wale wanaopokea washukuru kwa dhati kuwa umewafikia, licha ya kuwa ni kidogo uwafikie walengwa," alisema Ilomo.

Akipokea msaada huo mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Iringa Steven Mhapa ameushukuru mfuko huo huku akiwahakikishia wananchi  viongozi wake kutenda haki.

Mhapa alimtaka diwani wa Kata hiyo ya Izazi Tamson Sanga kujipanga ili kuhakikisha msaada huo unawafikia walengwa, na akimsisitiza diwani huyo kusimamia mwenyewe ugawaji wa vitu hivyo ili visichepushwe na kuzua lawama.

"Ninakushukuru sana katibu mkuu kwa msaada huu mliotupatia, na mimi niahidi kuwa msaada huu utaleta tija nikiwa na maana kuwa tutasimamia ipasavyo ili wananchi wetu, na mimi kama mwenyekiti wa halmashauri ninamuagiza diwani wa kata hii ya Izazi asimamie vilivyo ugawaji wa vitu hivi ili kusiwe na migogolo, na wananchi ninawaombeni muwe na amani kwani tumeleta misaada mbalimbali hapa na haijaleta lawama wala manung'uniko yoyote, ninawahakikishieni kuwa itawafikieni," Alisema Mhapa.

Hata hivyo Jasmin Luhala na Adam Msigala kwa niaba ya wananchi wameushukuru mfuko huo na serikali kwa ujumla kwa kuwasaidia kwa madai kuwa mali zao na baadhi ya vitu viliharibiwa vibaya na mvua hiyo iliyokuwa na upepo mkali.
MWISHO



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni