Jumatatu, 10 Februari 2014

WAFANYABIASHARA WAGOMA KUFUNGUA MADUKA


 Mtaa wa Uhindini moja ya mitaa ambayo siku za kawaida huwa na msongamano wa watu mjini Iringa.

 Mtaa wa Mantigo au Miyomboni kati ya mitaa ambayo nayo siku za kawaida huwa na msongamano mkubwa wa watu mjini Iringa.
 Hapa ni katikati ya mji wa Iringa- panaitwa mtaa wa Kongo, eneo la stendi ya daladala, nako hali ndiyo kama hii unavyoiona- maeneo haya huwa na mrundikano mkubwa wa watu mjini Iringa.

hapa ni eneo la barabara Pacha za Mwembetowa Stendi kuu, nako hali halisi kama inavyoonekana maduka nayo yamefungwa.

WAFANYABIASHARA mkoani Iringa wamegoma kufungua maduka, huku biashara mbalimbali za kiuchumi zikisitishwa, kwa kile wanachodai kuwa kufanyiwa usumbufu uliokithiri na baadhi ya watumishi wa wanaitaka Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA), zikiwemo mzigo wa kodi unaowaelemea.

Mgomo huo ambao umeanza mapema alfajiri ya siku ya leo, huku baadhi ya wanaofungua huduma za kibinadamu nao wakishinikizwa kutotoa  huduma hizo, unachangiwa pia na mashine za Kielectreonic za EFD za kutolea Stakabadhi pindi tu mteja anaponunua bidhaa .

Wakizungumzia mgomo huo baadhi ya wafanyabiashara hao wamesema mgomo huo umefikiwa baada ya kutosikilizwa kilio chao, huku kukiwa na mkanganyiko kati ya wafanyabiashara wa kariakoo jijini dar es salaam kusitishiwa utaratiubu huo mpya wa TRA wakati wao wa mikoani wanaonunua bidhaa zao zote kariakoo wakitakiwa kuwa na kumbukumbu za manunuzi.

"Hebu ona ndugu mwandishi, kule Kariakoo wanunuzi wanaotuuzia mali hizi zote kutokja mikoa wamepewa muda wa kuendelea na utaratibu wao wa zamani wa kutotumia mashine za EFD, lakini sasa sisi tunapokuja huku mikoani hawa TRA wanasema hawaelewi hilo tunatakiwa kuambatanisha kwenye malipo manunuzi yetu, sasa sisi tunatoa wapi wakati wafanyabiashara wakubwa dar hawatupi risiti??," Alihoji Tito Kalole.

James Mdegipala mmoja wa wafanyabiashara hao amesema ipo haja kwa TRA pia kuwasikiliza malalamiko yao juu ya gharama kubwa za ununuzi wa mashine hizo.


Makey Masharo amesema wataendesha mgomo huo mpaka malalamiko yao yatakaposikilizwa kwani baadhi ya wafanyabiashaea wameingiwa na hofu juu ya tishio la upandishaji wa kodi kwa  asilimia 18.


Jackson Kalole naye amesema serikali inapaswa kushirikiana na wadau wake pindi inapotaka kufanya mabadiliko, hasa yanayohusu uchumi wa nchi ili kuondokana na changamoto hizo, kwani licha ya kuwepo kwa kodi zaidi ya 9 kwa mfanyabiashara mdogo wa duka, kumekuwa na tatizo la elimu juu ya ongezeko la kodi hizo.

Aidha wafanyabiashara hao wamesema hawapo tayari kufungua maduka yao, hadi pale serikali itakapoona umuhimu wa kukaa meza moja na wao ili kumaliza changamoto hizo.


Naye Lukas Mwakabungu mwenyekiti wa chama cha wafanyabiashara, wenye viwanda na wakulima TCCIA amesema chemba hiyo haihusiki na mgomo huo na kuwa atakaa na wafanyabiashara hao ili kutambua sababu za wao kugoma.

Mkuu wa mkoa wa Iringa Dr. Christine Ishengoma amewataka wafanyabiashara hao kufungua maduka yao, kwa madai kuwa huo ni mkumbo wa baadhi ya vijana wanaochochea wenzao kutofungua maduka.

Hata hivyo wafanyabiashara hao wametawanywa na jeshi la polisi mara tu walipojaribu kutaka kukusanyana ili kujadili hatma ya tatizo hilo, ambapo wameitaka serikali kuona hasara inayoingia kwa kushindwa kukusanya kodi katika siku watakazokuwa wamesusia kufungua maduka na kutoa huduma kwa jamii.

MWISHO.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni