Jumamosi, 8 Machi 2014

WALEMAVU WALALAMIKIA KUTEGWA SIKU YA WANAWAKE



 Baadhi ya washiriki wa siku ya wanawake duniani wakipita katika barabara ya Mashinetatu mjini Iringa wakielekea uwanja wa Mwembetogwa kwa ajili ya maadhimisho ya siku hiyo.
 Baadhi ya wanawake wakioshiriki siku ya wanawake duniani wakielekea uwanja wa Mwembetogwa kwa ajili ya maadhimisho ya siku hiyo.
Baadhi ya washiriki wa siku ya wanawake duniani wakipita katika barabara ya Mashinetatu mjini Iringa wakielekea uwanja wa Mwembetogwa kwa ajili ya maadhimisho ya siku hiyo.

<<<HABARI>>>

WANAWAKE walemavu wa manispaa ya Iringa wamelalamikia hali ya kutoshirikishwa katika mipango ya siku hiyo, kwa madai kuwa hali hiyo inachangia wao kubaki nyuma katika siku hiyo muhimu kwao.

Walemavu hao wameyasema hayo katika uwanja wa Mwembetogwa wakati wa maadhimisho ya siku ya Mwanamke duniani ambapo Manispaa ya Iringa imeadhimisha katika uwanja huo,  ambapo Wanawake walioshiriki katika siku hiyo walivaa sare na walemavu hao kujikuta wakiwa wako tofauti na wenzao kwa kukosa sare.

Grace Dalu mmoja wa wanawake walemavu waliohudhuria sherehe hiyo, amesema Manispaa ilipaswa kuwashirikisha ili kuwa na muonekano mmoja katika sherehe hiyo, kuliko hali hiyo ambayo imeonekana kuwagawa.

Lukia Chagama amesema kumekuwa na matabaka katika kusherekea siku hiyo, huku wanawake walemavu hususani waishio maeneo ya pembezoni mwa mji siku hiyo wakiisikia katika vyombo vya habari pekee, jambo ambalo linawakosesha amani, wakati serikali inahimiza makundi maalumu  kushirikishwa katika masuala mbalimbali ya kijamii pasipo kubaguliwa.

Modesta Mkini katibu wa chama cha walemavu CHAWATA Wilaya ya Iringa licha ya tofauti iliyojitokeza katika siku ya wanawake, lakini kundi hilo la walemavu limekuwa halifikiwi hata na mikopo ya serikali ambayo imekuwa ikitengwa kwa ajili yao.

Mkini amesema mafungu ya fedha za walemavu kama yatawafikia moja kwa moja walemavu, basi wataweza kujikwamua na hali ngumu ya kiuchumi waliyonayo, kwa madai kuwa zingewawezesha shughuli za ujasiriamali.

Lakini katika siku hiyo ya wanawake, wanawake wenye ulemavu wameonekana idadi yao ni ndogo isiyozidi walemavu kumi jambo ambalo linaonekana kundi hilo kutoshirikishwa vya kutosha.

Afisa maendeleo wa Manispaa ya Iringa Susan Nyagawa anakiri kuwepo kwa changamomoto hiyo na kuwa mwaka unaofuata wanawake  wenye ulemavu watapewa kipaumbele kwa kushirikishwa moja kwa moja pamoja na kuwajali.
 
Hata hivyo wanawake hao wametoa misaada mbalimbali ya kujikimu kwa watoto yatima na waishio katika mazingira hatarishi ikiwa ni sehemu yao ya kuonyesha umuhimu wa kundi hilo la watoto katika jamii.

MWISHO

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni