Jumapili, 6 Julai 2014

TAMKO LA MAASKOFU KANISA KATOLIKI TANZANIA KWA BUNGE MAALUMU LA KATIBA (BMK).


 Rais wa maaskofu tanzania Askofu Ngalalekumtwa akisalimiana na rais mstaafu wa awamu ya tatu Benjamin Mkapa- katika jubilei ya miaka 25 ya Uaskofu na miaka 40 ya Upadre wa Ngalalekumtwa - sherehe zilizofanyika katika uwanja wa Kanisa la jimbo la Kihesa Iringa.

 Baadhi ya maaskofu.
 waziri mkuu Mizengo Pinda akimsalimu askofu Tarcisius Ngalalekumtwa- katika jubilei yake ya Uaskofu na Upadrisho, mjini Iringa.
 Waziri mkuu mstaafu- Edward Lowassa akisaliamiana na mmoja wa maaskofu katika jubilei ya askofu Ngalalekumtwa ambaye ni rais wa maaskofu Katoliki Tanzania.



 Askofu Ngalalekumtwa ambaye pia ni askofu wa jimbo la Kanisa Katholiki Iringa, akipokea zawadi siku ya jubilei yake- iliyofanyika katika jimbo la kanisa katholiki Kihesa-Iringa.




Jaji mstaafu Joseph Sinde Warioba akimkabidhi Rais Kikwete Rasimu ya pili ya katiba mpya.
KATIKA ujumbe wetu wa kichungaji wa Pasaka 2014, Sisi maaskofu Katoliki Tanzania, tuliwaandikia barua watu wote wenye mapenzi mema kwa nchi yetu tukiwaalika kuchukulia maanani mchakato wa kuandika Katiba mpya ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wakati huu tena tunawaalika Watanzania wote kwa pamoja, tuungane kuwakumbusha wale waliopewa dhamana yakukamilisha rasimu ya pili ya katiba ya jamuhuri ya muungano kuwajibika binafsi na katika maridhiano kutupatia Katiba Maridhawa.

Kwa moyo wa Sala na tafakarimakini, tulifuatilia mlivyojadiliana katika BMK kuanzia mwezi Februari hadi April 2014, katika siku sitini na saba (67)ninyi wateule wa Rais mpatao mia sita (600).

Mlijadiliana pasipo umoja, mkishambuliana kwa kauli kali kati yenu, mkikashfiana pasipo udhibiti wa uongozi mliojichagulia wenyewe kwa kanuni na sheria mlizojitungia.

Mwenendo huu ulikuwa wa kusikitisha na kuchukiza katika mahali pale panapoheshimiwa na wote, kwani tulitegemea majadiliano katika kuheshimiana hoja za kizalendo na kiungwana zitokanazo na mambo na masuala makuu yaliyopendekezwa katika Rasimu ya pili ya Katiba.

Badala yake tulijionea mabishano makali na mpasuko uliosababisha upotoshaji wa nia iliyokusudiwa, hatimaye hila na hilba zikateka kabisa jukumu adili la BMK.

Tukumbuke Rais wa jamuhuri ya muungano wa Tanzania kwa uthubutu na ujasiri wa kipekee,  alianzisha machakato wa kuunda katiba mpya, na kisha aliridhia kwa kuipokea rasmi kwa furaha Rasimu ya pili ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Ni lazima sasa tujiulize, nini kimetokea hadi kugeuza kabisa mwelekeo mzima wa mchakato wa katiba kwa kuikejeri na kushutumu vikali Rasimu hiyo katika wakati wa kipekee kabisa wa kihistoria wa uzinduzi wa BMK? Hata kusahau gharama kubwa ambayo ilibebwa na walipa kodi? Na sasa hii inaonyesha dhahiri jambo hili limeiingiza nchi katika mgogolo mkubwa unaoashiria hatari mbeleni.

Kwa maoni yetu tatizo hili kubwa ambalo limekuwa kikwazo kikubwa linaonyesha kukosekana utashi wa kisiasa na wahusika kutokuwa wakweli juu ya suala la mchakato wa katiba.

Tunawaomba wajumbe wa BMK kuwa wamoja na kufanya kazi yenu kwa mtazamo usioegemea siasa za vyama kuandika katiba ni kazi iliyo ngazi ya juu zaidi ya siasa za vyama na hivyo utashi wa kisiasa wa kuunda katiba mpya wa kuzingatia msingi huu.

Kwa kadri ya hali ya nchi yetu ziko sababu za kutosha za kutaka katiba mpya Sababu hizi ni pamoja na ufisadi, wananchi kujisikia kukosa usalama, nchi kutokuwa na dira, tunu, msingi n.k.

Ni kwa hiyo tunawasihi kwa mara nyingine tena ninyi wajumbe wa BMK kurejea katika sehemu ya pili ya mjadala hapo mwezi August mkiwa na moyo na mtazamo mpya.

Tunaomba achaneni kabisa na ubinafsi, uwe wa mtu mmoja mmoja au katika vikundi. Kwa kazi yenu tusaidieni sisi watanzania tuweze kujivunia kuwa na Taifa adilifu tukifanyakazi kwa pamoja kwa ajili ya manufaa na ustawi wa wote.

Kumbukeni BMK mnao wajibu wa kimaadili kwa nchi yetu na vile kwa namna mnavyotekeleza wajibu wenu maandika historia ya nchi yetu, kubeba dhamana ya kuandika katiba mpya ni wajibu wa kimaadili kwenu.

Tambueni kwamba Watanzania hawako tayari kurudi nyuma na kuendelea na maisha yanayoongozwa na katiba ya mwaka 1977 kwa sababu licha ya mapungufu yake na ukiukwaji mkubwa ambao umekuwa ukifanyika, kufanya hivyo (Kuendelea kuongozwa na katiba ya 1977) kutaleta migogolo mikubwa yenye kuhatarisha vikali amani nchini.

Wajibu mliokabidhiwa ikiwa mtautimiza kwa dhamira njema mtalijengea Taifa letu misingi imara iliosheheni tunu za kimaadili ambazo ni heshima katika utu wa Mwanadamu, umoja, mshkamano na kujali na manufaa na ustawi wa wote.

Ni lazima matunda ya kazi yenu yawe ni kulipatia Taifa dira inayowapa watu msukumo wa kujenga pamoja Taifa lenye watu wamoja na wanaojaliana kwa stahamala katika tofauti zao.

Wajibu wenu huo ni mtakatifu na hivyo ni kosa kubwa mno kuusaliti kwa sababu ya ushindani katika medani za kisiasa au kujitafutia sifa mbele ya watu.

Kwa matokeo yoyote yatakayotokana na kazi yenu katika BMK Watanzania watawawajibisha, ikiwa matokeo yatakuwa yenye kuleta mema na kuimarisha amani na utulivu nchini watu wote watawashukuru na kuwasifu.

Lakini kama tunda la kazi yenu litakuwa ni lenye kuiingiza nchi katika matatizo zaidi, kuwataabisha wananchi na kukosa maelewano baina yao, basi watu watawahukumu na kuwawajibisha kwa kukosa umakini katika jukumu hili muhimu mlilokabidhiwa.

Kwa sasa tunahitaji Katiba itakayowezesha ushiriki kamili wa watu katika maamuzi ya vipaumbele vya maendeleo yao ya Taifa. Ni katiba shirikishi katika matumizi ya madaraka ili yatumike kwa ajili ya kuhudumia wote badala ya wachache.

Tunahitaji katia ambayo inaruhusu utawala wa sheria, haki sawa kwa wote, manufaa na ustawi kwa wote na kuheshimu Utu wa kila mmoja, Katiba iwezayo kuzuia matumizi mabaya ya madaraka na Ufusadi, hicho ndicho wananchi wanachokitarajia kutoka kwenu.

Yeyote anayedharau hitaji la katiba mpya ama anayejaribu kupuuza na kuweka kando Rasimu ya pili, huyo siyo mwakirishi wa utashi wa watu, mwisho wake Historia itamuhukumu vikali mtu huyo.
Wajumbe wa BMK msiwaangushe watu wenu.

Sisi Maaskofu Katoliki Tanzania tunawaahidi sala zetu ili mwenyezi Mungu awaangazie Nuru yake na kuwajalia nguvu ya KiMungu muweze kukamilisha kazi kwa mafanikio kadiri ya matarajio ya watu wake wa Tanzania.

Tunawaalika watu wote wenye mapenzi mema kuwaombea wajumbe hao na bunge maalumu la katiba wajaliwe neema za Mungu.

T. Ngalalekumtwa.
MWISHO

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni